Moduli hii inalenga kumpa mwanafunzi uelewa wa kina katika nyanja za Isimu Linganishi na Anthropolojia ya Kiswahili. Hivyo, moduli hii inakusudia kumwezesha mwanafunzi kukuza umahiri wa kulinganisha, kulinganua na kuchambua lugha za Kibantu kwa kuzingatia vipengele vya kimuundo, kiuamilifu na kiutamaduni.
Aidha, kupitia mbinu za isimu historia linganishi, mwanafunzi ataendeleza uwezo wake wa kiisimu kwa kuchunguza asili, maendeleo na miundo ya Kiswahili. Katika mchakato huu, ataweza kulinganisha Kiswahili na lugha nyingine za Kibantu, hususan Kinyarwanda, ili kuimarisha maarifa na stadi zake za uchambuzi na matumizi ya lugha katika ufundishaji wa Kiswahili katika miktadha mbalimbali ya kielimu.
Kwa msingi huo, moduli hii itamwezesha mwanafunzi kuchunguza kwa kina na kufafanua uhusiano uliopo kati ya lugha na utamaduni, na hivyo kuimarisha uelewa wa matumizi ya lugha katika mazingira tofauti ya kijamii na kitaaluma.